Sunday, March 18, 2012

Uchomvu isiwe sababu ya kunyimana ‘chakula cha usiku’

Ndani ya maisha ya ndoa, muda wowote mwenzako anapohitaji penzi hutakiwi kumkatalia kwa kuwa wewe ndiye daktari wake na kumkubalia kwako ni sawa na kumtibu ugonjwa ambao ungeweza kuyaathiri maisha yake.

Hata hivyo, asilimia kubwa ya wanandoa wanatajwa kufanya tendo la ndoa wakati wa usiku. Usiku wa saa ngapi? Hiyo itategemea na wanandoa husika.

Lakini sasa inaelezwa kuwa wanandoa wanaofanya kazi ni vigumu sana kulifurahia tendo la ndoa kwa kulifanya usiku. Hii ni kwa sababu, muda huo kila mmoja anakuwa amechoka kutokana na mihangaiko ya siku nzima.

Usiku ni tatizo?

Wanaume wengi wakati wa usiku ndiyo wanautumia kutafakari juu ya maisha, pia ni wakati ambao wanakuwa wamechoka hivyo wanaweza kukosa mshawasha wa kukutana na wake zao.

Ukijaribu kufuatilia utabaini ndoa nyingi ziko kwenye migogoro chanzo kikiwa na wanawake kutopatiwa haki zao za ndoa. Wanaikosa haki hiyo kwa kuwa muda ambao waume zao wanatakiwa kuwapa ‘mambo’, wanakuwa hoi.

Mbaya zaidi baadhi ya wanawake hufikia hatua ya kuhisi wanasalitiwa kumbe siyo kweli bali inatokana na kutopatiwa raha hiyo kwa wakati walioutarajia.

Wataalam wa mapenzi wanaeleza kuwa, usiku ndiyo muda muafaka kwa wanandoa kukutana na kwa mwanaume hata kama atakuwa anajisikia hali ya kuchoka, ajue ana wajibu wa kufanya hivyo.

Kufanya mapenzi ni moja ya mazoezi hivyo mwanaume anaporudi nyumbani asikimbilie kuoga, kula na kulala bali akumbuke kumpatia haki mke wake, haki ambayo pia inamsaidia kimazoezi.

Inaelezwa kuwa, mwanaume kujihisi uchovu kila siku na kushindwa kufanya tendo la ndoa ni dalili kwamba ana tatizo la kiafya analotakiwa kulitafutia ufumbuzi haraka kabla ya kuiathiri ndoa yake.

Mapenzi ni starehe

Ifahamike kwamba, kufanya mapenzi licha ya kwamba unatumia nguvu na akili lakini ni sehemu ya kustarehe. Ndiyo maana wengine baada ya kumaliza shughuli zao za siku nzima badala ya kwenda baa, moja kwa moja wanakwenda nyumbani na wakifika huko wakioga wanaweza kutumia muda mwingi kitandani na wenza wao.

Kwa maana hiyo kukutana faragha isichukuliwe kama kitu kitakachokufanya uzidi kuchoka bali kwa kutumia kanuni sahihi, uchovu hauwezi kuwa sababu ya kutomtimizia mwenzake haki yake ya ndoa.

Mwanaume afanyeje?

Zipo njia mbalimbali za kukabiliana na hali ya uchovu na leo nitazungumzia mbili ambazo naamini ukizifanyia kazi zinaweza kukusaidia.

Kunywa kahawa

Wapo wanaoitumia kama njia ya kuwafanya wasilale usiku lakini pia kitaalam inaelezwa mtu anapokunywa kahawa kabla ya kupanda kitandani inamsaidia kuondoa uchovu.

Aidha, kahawa ina uwezo wa kumfanya mtu apate mshawasha wa kufanya tendo la ndoa hata kama ametoka kwenye kazi zilizomfanya achoke sana.

Mazingira ya kutokuwa mchovu yatamfanya aweze kumtimizia mke wake haki yake ya ndoa bila wasiwasi. Cha kuzingatia katika hili ni kunywa kahawa kiasi ili isikuletee madhara badala ya faida.

Tumia zabibu za baridi

Wataalam wanaeleza kuwa, zabibu hasa za baridi zinaweza kukuweka katika mazingira mazuri ya kukutana faragha na mwenzako na kushibishana chakula cha usiku.

Ukiwasili nyumbani kutoka kazini na kuhisi hali ya kuchoka. Baada ya kuoga ukiwa umepumzika kula tunda hilo taratibu, faida yake utaiona utakapokuwa kitandani na mwenza wako.

Zingatio

Kukutana faragha ni mhimili muhimu katika kuidumisha ndoa. Visingizio visivyo na msingi visitumike kunyimana utamu huu. Kama umechoka basi ujue ukifanya mapenzi na mwenzako uchovu utaondoka, kama hujisikii kufanya hivyo mwenzako atakupa stimu lakini usipuuzie hisia zake.

No comments:

Post a Comment