Sunday, March 18, 2012

Mtu Mwenye Mioyo Miwili apata Mishtuko ya Mioyo na Kupona

Mtu Mwenye Mioyo Miwili
Raia mmoja nchini Italia mwenye umri wa miaka 71 alipata mishtuko ya mioyo yake yote miwili na kupoteza fahamu kwa sekunde kadhaa lakini hatimaye aliweza kuokolewa maisha yake. Mtu huyo alikimbizwa katika hospitali ya Verona nchini Italia baada ya kupata maumivu ya kifua na mapigo ya mioyo yake kuwa si ya kawaida.

Taarifa kutoka jarida la American Emergency Medical Journal inaeleza kuwa mtu huyo aliwahi kufanyiwa upasuaji wa moyo na kupandikizwa moyo mwingine miaka kadhaa iliyopita katika upasuaji unaojulikana kama double heart transplant (heterotopic heart transplantation). Hii ni aina ya upasuaji ambapo moyo hupandikizwa na kufanya kazi sambamba na moyo wa awali (wa mgonjwa mwenyewe) ambao huwa umeadhirika kutokana na maradhi. Chemba za damu za kwenye mioyo hiyo huunganishwa ili moyo uliopandikizwa uweze kusaidia moyo wa mgonjwa.
Ripoti zinasema kuwa moyo mmoja ulianza kuwa na nguvu zaidi kuliko mwingine na hivyo kusababisha mapigo yake kutofautiana na mwingine. Madaktari walijaribu kurekebisha mapigo ya mioyo hiyo ili yaendane sawa kwa kutumia dawa lakini mioyo hiyo iliacha kupiga kabisa na mtu huyo kuacha kupumua. Hata hivyo, waliweza kumrejesha katika hali ya kupumua kwa kutumia kifaa maalum cha Defibrillator kabla ya kumfanyia upasuaji na kubadilisha kifaa kinachosaidia kuweka sawa mapigo ya moyo kinachojulikana kama pacemaker.
Mtu huyo ambaye bado ana mioyo hiyo miwili, yupo hai na afya yake ni nzuri tangu alipofanyiwa upasuaji huo mwaka 2010.
Dk Giacomo Mugnai ambaye alihusika katika kumtibu mtu huyo anakiri kupitia barua pepe aliyotuma kwenda kwa mtandao wa msnbc.com kuwa hawajawahi kuona mgonjwa kama huyo hapo awali.
Dk Rade Vukmir, Profesa wa kitengo cha tiba ya dharura (Emergency Medicine) wa Chuo Kikuu cha America’s Temple University na msemaji wa American College of Royal Physicians anasema amewahi kushuhudia namna hiyo ya upasuaji ikifanywa katika moyo na figo huko nyuma.
Madaktari wa upasuaji kawaida huacha figo au moyo katika sehemu yake ya kawaida na kupandikiza mwingine ikiwa figo/moyo huo utakuwa kazi kubwa sana kutoa, au kama kuna matarajio ya figo/moyo huo kupona hapo siku za usoni ikiwa utasaidiwa na figo/moyo wa kupandikizwa.
Aina hii ya upasuaji (double heart transplant) ni nadra sana siku hizi kutokana na vifaa maalum ambavyo vingesaidia moyo huu wa pili wa kupandikizwa vinavyojulikana kama Ventricular Assist Devices ambavyo vilikuwa vikubwa sana na ghali miaka 20 iliyopita kuwa ni vidogo na rahisi kuvibeba katika miaka ya hivi karibuni.
Watu wanaofanyiwa upasuaji huu huishi kwa wastani wa miaka 15 baada ya kuwekea moyo wa pili lakini mtu atahitaji kufundishwa jinsi ya kuishi na moyo mwingine wa ziada, kuhudhuria hospitali mara kwa mara kuangaliwa maendeleo yake pamoja na kutumia dawa kwa muda mrefu.

No comments:

Post a Comment