Sunday, March 18, 2012

Mafua ya Ndege

Huu ni ugonjwa unaoathiri zaidi ndege wa jamii mbalimbali. Hata hivyo virusi wanaosababisha ugonjwa huu, wana uwezo wa kujibadilisha umbo na tabia zake (mutation) na kisha kumuathiri mwanadamu. Mabadiliko haya ya kimaumbile na kitabia husababisha kutokea kwa milipuko (epidemic) ya mafua ya ndege sehemu mbalimbali duniani hali ambayo isipothibitiwa inaweza kusambaa na kuathiri sehemu kubwa ya dunia kwa wakati mmoja (pandemic).

Visababishi vya mafua ya ndege
Mafua ya ndege husababishwa na jamii ya virus wajulikanao kama Avian Influenza virus. Virusi vya kwanza kabisa kumuathiri binadamu na kumsababishia mafua ya ndege vilihusishwa na kuku na viligunduliwa mwaka 1997 huko nchini Hong Kong na kupewa jina la avian influenza A (H5N1). Huu ulikuwa ni mlipuko wa kwanza wa ugonjwa huu kuwahi kuripotiwa. Kuna matukio machache sana ya maambukizi kutoka kwa binadamu kwenda binadamu yaliyowahi kuripotiwa mpaka sasa.

Influenza virus ni nini?
Kuna aina kuu tatu za virusi wa influenza, A, B na C. Mafua ya ndege husababishwa na jamii ya influenza A ambao wana uwezo wa kuingia na kuishi katika seli za ndege. Umbo la kinasaba la virusi hawa wa influenza A limeundwa na kamba nane za protein aina ya RNA. Aidha virus wa Influenza wanaweza pia kuainishwa kulingana na aina ya protein inayounda maumbo yao. Protini hizo zipo katika aina mbili nazo ni hemagglutinin (H) pamoja na neuraminidase (N). Protini hizi zina kazi mbalimbali katika umbo la virusi. Kadhalika protini hizi nao pia zimeganyika katika aina mbali, ambapo virusi hatari wa mafua ya ndege wanaundwa na aina ya 5 ya protin ya hemagglutinin na aina ya 1 ya protini ya neuraminidase na hivyo ndiyo maana hujulikana kama H5N1 influenza A virus.

Wapo virusi wa influenza ambao huishi katika mwili wa binadamu tu, hawa hujulikana kama human influenza; na wapo wengine ambao huishi katika miili ya wanyama kama vile nguruwe, chui, na hata paka. Hata hivyo wakati fulani, muingiliano kati ya virusi hawa na wenyeji wao yaani waathirika hutokea.

Ukubwa wa tatizo
Tangu hapo, matukio kadhaa ya milipuko ya ugonjwa wa mafua ya ndege kwa binadamu inayohusishwa na virusi wa avian influenza A (H5N1) yamepata kuripotiwa katika sehemu kadhaa za mabara ya Asia, Afrika, Ulaya na pia nchi za Vietnam, Indonesia, na maeneo kadhaa ya Mashariki ya mbali. Mamia ya watu wameripotiwa kufa kutokana na milipuko hiyo ambapo inakadiriwa kuwa zaidi ya asilimia 60 ya watu wote waliopatwa na ugonjwa huu walifariki dunia.

Vihatarishi vya ugonjwa wa mafua ya ndege
Kadiri jinsi virusi wa mafua ya ndege wanavyosambaa ndivyo uwezekano wa kutokea kwa milipuko ya ugonjwa huu inayoathiri binadamu sehemu mbalimbali duniani unavyokuwa mkubwa. Watafiti wameonesha kuwepo kwa hatari ya kutokea kwa mlipuko mkubwa (pandemic) unaoweza kusababishwa na kusambaa kwa virusi hawa duniani.

Watu walio katika hatari ya kukumbwa na ugonjwa wa mafua ya ndege ni pamoja na:
• Wakulima na wale wanaojishughulisha na ufugaji wa jamii mbalimbali za ndege
• Wasafiri wanaotembelea maeneo yaliyokumbwa na mlipuko
• Yeyote anayegusa ndege aliyeathirika na mafua ya ndege
• Mtu anayekula nyama
ya ndege aliyeambukizwa virusi wa avian influenza ikiwa mbichi au isiyoiva vizuri au kula mayai au damu za ndege wenye virusi hao
• Aidha, watoa huduma za afya pamoja na ndugu za wagonjwa wenye ugonjwa huu nao pia wapo katika hatari kubwa ya kupata maambukizi ya mafua ya ndege.

Imeonekana kuwa virusi wa avian flu virus (H5N1) wana uwezo mkubwa wa kuishi katika mazingira kwa muda mrefu bila kuathirika. Katika hali hii, maambukizi yanaweza pia kusababishwa na mtu kugusa maeneo walipo virusi hawa.

Ndege walioambukizwa ugonjwa huu huendelea kutoa virusi kupitia katika vinyesi vyao au mate yao kwa muda wa mpaka siku kumi tangu waambukizwe.

Dalili za mafua ya ndege
Dalili za mafua ya ndege kwa binadamu hutegemeana na aina ya virusi waliomshambulia muhusika. Dalili pia zinaweza kuanza kujitokeza siku saba mpaka kumi tangu mtu anapopatwa na maambukizi ya virusi wa H5N1.
Maambukizi yanayosababishwa na virusi vya jamii ya H5N1 kwa binadamu husababisha mgonjwa kuwa na dalili zote za mafua makali kama vile
• kukohoa (kikohozi kikavu au wakati mwingine kinachotoa makohozi),
• kuharisha sana,
• kutapika
• kichefuchefu
• kupumua kwa shida, (Acute Respiratory Distress Syndrome)
• homa zaidi ya nyuzijoto 38 centigrade,
• kuumwa na kichwa,
• kujihisi uchovu wa mwili,
• maumivu ya misuli ya mwili mzima,
• kutokwa na makamasi mepesi yanayotiririka bila ukomo na
• kuwashwa na koo.

Vipimo na uchunguzi
Kabla daktari hajaagiza kufanyika kwa vipimo, anaweza kwanza kutaka kujua historia ya mgonjwa ili kufahamu dalili zinazomsumbua. Kisha atamchunguza mgonjwa kwa kumpima kifua (kusikiliza sauti za hewa zinazoingia na kutoka katika mfumo wa njia ya hewa), kumpima joto la mwili, na pia kuchunguza pua na koo.

Baada ya uchunguzi wa mwili, daktari anaweza kuagiza vipimo vifuatavyo kufanyika.

  • X-ray ya kifua ili kuchunguza iwapo kuna athari zozote katika mapafu,
  • kuchukua sehemu ya makamasi na makohozi kutoka kwenye koo na pua yaani nasopharyngeal culture na kuotesha maabara ili kufahamu aina ya virusi na bakteria wanaomsumbua mgonjwa
  • kipimo cha damu yaani Full Blood Picture mkazo ukiwekwa kwenye kuangalia chmbe nyeupe za damu kama zipo sawa au zimeongezeka,
  • vipimo vya utendaji kazi wa mafigo, ini pamoja na moyo pia ni muhimu kufanyika.

Ingawa vipimo vya kutambua virusi wa mafua ya ndege kama vile PCR vipo, lakini havijasambaa sehemu nyingi duniani. Hata hivyo, vipimo hivi hutumia muda mfupi sana (chini ya saa tano) kutoa majibu ya kutambua jamii ya virusi inayomuathiri mgonjwa na hivyo kumuwia urahisi tabibu kushughulika navyo.

Matibabu
Kama tulivyoona hapo juu kuwa, jamii mbalimbali za virusi wa avian flu huweza kusababisha dalili tofauti tofauti. Hivyo basi hata matibabu pia yaweza kutofautiana kati ya mgonjwa na mgonjwa.

Kwa ujumla, iwapo ndani ya saa 48 tangu kujitokeza kwa dalili, mgonjwa atapatiwa dawa za kuua virusi za aina ya zanamir au oseltamivir kuna uwezekano mkubwa wa kupunguza makali ya ugonjwa na hivyo kuongeza uwezekano wa mgonjwa kupona.

Pia ndugu na jamaa wanaoishi nyumba moja na mgonjwa wanaweza kupewa dawa ya Oseltamivir ili kuwakinga wasipatwe na maambukizi ya virusi hawa, na iwapo watakuwa wameambukizwa, kuwaua kabla hawajasambaa zaidi mwilini.

Dawa za amantadine na rimantadine ambazo hutumiwa mara kwa mara kwa ajili ya kutibu maambukizi ya aina mbalimbali za virusi imeonekana kuwa hayana uwezo wa kuua virusi wanaosababisha mafua ya ndege na hivyo inshauriwa kutoyatumia pindi mlipuko wa mafua ya ndege unapotokea.

Baadhi ya wagonjwa wanaweza kuwa na hali mbaya sana kuliko wengine. Wapo ambao hufikia hatua ya kushindwa kupumua wenyewe. Wagonjwa wa namna hii hawana budi kulazwa katika vyumba vya uangalizi maalum na kusaidiwa kupumua kwa kutumia mashine. Aidha inashauriwa sana na wataalamu wa magonjwa ya mlipuko kuwatenga wagonjwa wote wa mafua ya ndege katika sehemu maalum ili kuzuia kusambaa zaidi kwa ugonjwa huu.

Chanjo dhidi ya mafua ya ndege
Watafiti wamefanikiwa kutengeneza chanjo dhidi ya virusi wanaosambaza ugonjwa wa mafua ya ndege. Chanjo hiyo ambayo imethibitishwa na mamlaka mbalimbali za madawa duniani imetengenezwa kwa lengo la kumkinga binadamu dhidi ya maambukizi ya mafua ya ndege na inaweza kutumika iwapo virusi wa H5N1 atabdilika tabia na kuanza kusambaa kutoka kwa binadamu kwenda kwa binadamu mwingine.

Kadhalika, wataalamu wanashauri sana watu kupata chanjo dhidi ya virusi wa influenza (wale wanaosababisha mafua ya kawaida kwa binadamu) ili kupunguza uwezekano wa virusi wa mafua ya ndege kujichanganya na virusi wa mafua ya kawaida (yaani human influenza) na kuzaa virusi wapya ambao wanaweza kuwa na uwezo wa kusambaa kwa urahisi zaidi na kuwa hatari zaidi kuliko hawa waliopo sasa.

Matarajio
Matokeo ya ugonjwa hutegemea sana ukali wa maambukizi pamoja na aina ya virusi waliomshambulia mgonjwa. Ikumbukwe kuwa karibu nusu ya wagonjwa wanaopatwa na mafua ya ndege hufariki.

Madhara
Madhara ya ugonjwa wa mafua ya ndege ni pamoja na
• Kupata shida wakati wa kupumua (Acute Respiratory Distress)
• Kushindwa kufanya kazi kwa viungo mbalimbali vya mwili (multi-organs failure)
• Homa ya mapafu
• Maambukizi katika damu (septicemia)

Kinga
Inashauriwa sana kuepuka njia zote ambazo zinaweza kukufanya upate maambukizi ya ugonjwa huu. Njia hizo ni pamoja na
• Kwa wasafiri, ni muhimu kuepuka kutembelea maeneo wanapouzwa au kufungwa ndege hususani sehemu zilizoripotiwa au kuhisiwa kuwa na milipuko ya ugonjwa huu
• Wafugaji wa ndege wanaohisiwa kuwa na virusi vya mafua ya ndege wanapaswa kuvaa vifaa maalum vya kujikinga ili wasipatwe na maambukizi
• Nawa mikono kwa sabuni mara baada ya kushika ndege au mazao ya ndege wenye maambukizi
• Inashauriwa kuepuka kula nyama mbichi au isiyoiva vizuri ya ndege (kuku, bata, njiwa) ili kupunguza uwezekano wa maambukizi
• Iwapo utaamua kupika nyama ya ndege, hakikisha unaipika katika nyuzijoto si chini ya 165 Farenheit
• Epuka kugusa ndege au mazao ya ndege (vinyesi, damu, mayai) wanaohisiwa kuwa na virusi vya H5N1
• Nenda hospitali haraka iwapo utajihisi kuwa na dalili za mafua ya ndege (kama zilivyotajwa hapo juu) ndani ya siku kumi baada ya kushika ndege au mazao ya ndege wanaohisiwa kuwa na virusi vya H5N1 au iwapo ulisafiri kwenda eneo lenye mlipuko wa mafua ya ndege.
• Epuka kunywa dawa za kuua virusi wa mafua ya ndege bila kupata ushauri wa daktari.

No comments:

Post a Comment