Sunday, March 18, 2012

Jinsi ya Kuandaa Chakula cha Mtoto

 Chakula cha Mtoto

Mtoto ale chakula muda gani?

Chai ya asubuhi: Saa 12:00 mpaka 2:00 kutegemeana na ni muda gani mtoto anakwenda shule. Jambo la muhimu ni kuwa, mzazi/mlezi ahakikishe mtoto anakula asubuhi ili asiende shle akiwa na njaa, ikibidi mzazi/mlezi amfungie mtoto chakula abebe.

Chakula cha mchana: Muda wa kati ya saa 5:30 mpaka saa 7:00 mchana.

Chakula cha jioni: Saa 10:00

Chakula cha usiku: Saa 1:00 usiku

Jinsi ya kuandaa chakula cha siku ya Jumatatu

Asubuhi: Kifungua kinywa (Breakfast)

Mlo 1: Chapati Maji Na Juisi Ya Chungwa

Mahitaji: 250 gram Unga wa ngano, 1 yai, 100 gram maziwa ya maji, 20 gram mafuta ya mahindi, 10 gram baking powder

Jinsi ya kuandaa chapati maji: Changanya vitu vyote katika bakuli kisha piga na mchapo mpaka upate mchanganyiko safi na laini kabisa. Iwapo mchanganyiko bado mzito ongeza maji kiasi.

Jinsi ya kuandaa juisi ya chungwa: Menya chungwa safi kabisa ili kuondoa uchungu wa gesi iliyopo katika maganda. Kisha tumia chombo maalumu cha kukamulia juice, kamua kisha hifadhi katika friji bila kuweka sukari ili ikae kwa muda bila kuharibika. Kumbuka pia kuweka sukari wakati wa kunywa.

Mlo 2: Uji wa Ulezi na Mtindi

Mahitaji: 200 gram unga wa ulezi, 100 gram maziwa ya maji, 350 gram maji, 100 gram mtindi usio na ladha ya matunda

Jinsi ya kuandaa uji wa ulzei na mtindi: Changanya unga wa ulezi na maziwa katika bakuli kisha chukua sufuria weka maji kiasi cha gram 350. Chemsha maji yakishachemka weka mchanganyiko wa maziwa na unga wa ulezi koroga mpaka uchemke na kuchanganyika safi kabisa ili uji wako usishike chini na kuungua. Acha uchemke vizuri kisha onja ukipata ladha ya kuiva kwa nafaka utakua tayari.

Toa jikoni weka katika bakuli litakalotumiwa na mtoto kisha changanya mtindi usio na ladha ya matunda pamoja na sukari tayari kwa mtoto kunywa.

Mchana: Chakula cha mchana

Mlo: Glass ya maziwa na mkate wa nyama za kusindika

Jinsi ya kuandaa: Mpatie mtoto 200 gram za maziwa sawa na glasi moja ya uvuguvugu au ya baridi lakini kumbuka yawe yamechemshwa vizuri na yakapoa kwa ajili ya usalama.

Kisha chukua vipande viwili vya mkate paka siagi au mayonaisi. Kisha chukua beef salami na beef backon weka kati kati pamoja na slice ya nyanya na tango mbichi mpatie mtoto ale.

Jioni: Chakula cha jioni

Mlo: Sahani ya mchanganyiko wa mboga mbichi

Jinsi ya kuandaa: Chukua caroti, tango, pilipili hoho nyekundu na ya kijani zote mbichi na zuchini ichemshe kidogo kisha weka mtindi wenye ladha ya matunda kwa ajili ya kulia hizo mboga

Huu ndio muonekano wa sahani ya mchanganyiko wa mboga kama mtoto ni mdogo sana zisage kwenye mashine ya kusagia nyama kisha utapata mchanganyiko laini mpatie mtoto asiyeweza kutafuna hizo mboga mbichi.

Usiku: Chakula cha usiku

Mlo 1: Supu ya uyoga

Mahitaji: 300gram Uyoga fresh au wa kopo, 50 gram kitunguu maji, 10 gram kitunguu swaumu, 10 gram tangawizi, 50 gram leeks, 100 gram viazi mbatata, 100 gram maziwa fresh, 50 gram mafuta ya kupikia, 300 gram maji

Jinsi ya kuandaa supu ya uyoga: Kaanga katika mafuta ya kupikia vitunguu maji na vitunguu swaumu pamoja na tangawizi. Kisha weka viazi mbatata, leeks na uyoga kaanga tena kiasi kisha weka maziwa na maji acha ichemke mpaka viazi viive kisha toa na saga kwenye blenda. Rudisha jikoni kama itakuwa nzito sana ongeza maziwa au maji kiasi. Usisahau kuweka chumvi kulingana na ladha.

Mlo 2: Kuku maziwa, muhogo na njegere

Mahitaji: 200 gram nyama ya kuku isiyo na mifupa, 100 gram njegere, 200 gram maziwa, 150 mihogo iliyochemshwa kwanza, 300 gram maji

Kulia ni machine ya kusagia nyama utakayoitumia kwa ajili ya kusagia vyakula mbali mbali.

Jinsi ya kuandaa kuku maziwa, muhogo na njegere: Chemsha vyote kwa pamoja kuku na njegere mbichi pamoja na muhogo uliokwisha chemshwa kwanza mpaka ikaribie kukauka mchuzi kisha toa jikoni. Chuja kisha weka mchuzi pembeni.

Chukua mchanganyiko wa njegere, kuku na muhogo. Tumia machine ya kusagia nyama weka huo mchanganyiko kisha saga upate rojo zito kisha rudisha katika sufuri, changanya na ule mchuzi uliochuja ongeza chumvi kulingana na ladha mpe mtoto ale chakula kikiwa cha moto.

Kama huna mashine ya kusagia nyama tumia mwiko kuponda itakua safi kabisa kisha unachanganya na ule mchuzi uliochuja.

Kwa mtoto mkubwa usisage. Baada ya kuchemsha ikaiva ongeza chumvi kisha mpakulie ale chakula cha moto atafurahia sana mchanganyiko wa ladha ya chakula hiki.

Orodha kwa ajili ya manunuzi siku ya Jumatatu

Uyoga wa kopo au fresh, mihogo mibichi, pili pili hoho, tangawizi, unga wa ngano, mayai, maziwa, sukari, chumvi, njegere, nyama ya kuku, tango, zucchini, mtindi usio na ladha ya matunda, mtindi wa ladha ya matunda, baking powder, viazi mbatata, mafuta ya mahindi na leeks.

Vitu hivi vyote sio vingi na unaweza kuvitumia siku inayofuata maana menu yetu ina uwiano safi kabisa. Vitu vingi vinatumika karibu kila siku na manunuzi yake sio ghali kabisa. Mpe mwanao raha kwa kula chakula safi na salama.

No comments:

Post a Comment